Friday 18 July 2014

Ferdinand ajiunga na QPR


Difenda wa zamani wa Manchester United Rio Ferdinand alijiunga na vijana wageni Ligi ya Premia QPR bila ada yoyote Alhamisi na akafichua kwamba alikataa ofa za kuvutia zaidi ili arudi London.
Ferdinand alikubaliana mkataba wa mwaka mmoja na klabu hiyo, na kuhitimisha harakati zake za kusaka klabu mpya baada ya kuachiliwa huru na United kufuatia kumalizika kwa mkataba wake mwezi jana.
Mchezaji huyo wa miaka 35 alitaka sana kurudi London, alikozaliwa na amekubali kujiunga tena na mdosi wa QPR Harry Redknapp, aliyempa fursa ya kucheza mechi ya kwanza ya ushindani walipofanya kazi pamoja West Ham.
Ferdinand alifichua hamu yake ya kuchezea klabu aliyoienzi akiwa mvulana mdogo ndiyo iliyomfanya kuhamia Loftus Road, ambako kakae Anton na binamu Les walicheza na kuvuma sana.
"Nilizoea kukaa na kutazama wakicheza, babangu alizoea kunileta hapa nikiwa mvulana mdogo. Kuna kumbukumbu kuu sana kwangu hapa na kwa familia yangu,” Ferdinand aliambia tovuti ya QPR.
"Anton alikuwa na mema pekee ya kusema kuhusu QPR na nilimtazama Les (Ferdinand) akicheza hapa nikiwa mvulana mdogo, pamoja na kina Ray Wilkins, Clive Wilson, David Bardsley naAlan McDonald."
Ferdinand, aliyeshinda mataji sita ya Ligi ya Premia na Ligi ya Klabu Bingwa 2008 wakati wa kipindi cha miaka 12 alichokaa United, ndiye mchezaji wa kwanza kununuliwa na Redknapp kipindi hiki cha kabla ya msimu, baada yake kuongoza QPR kurudi tena Ligi ya Premia kupitia mechi ya muondoano ya baada ya msimu katika ligi ya Championship.
Redknapp hana shaka kwamba Ferdinand anaweza kucheza vyema soka ya ligi kuu licha yake kutocheza vyema sana akiwa United msimu uliopita.
"Rio ni mchezaji mzuri sana na msakata gozi stadi. Nina furaha kwamba tumeweza kumleta hapa,” akasema Redknapp.
"Nilimchukua Rio akiwa mvulana wa miaka 14. Alitamba uwanjani nan je ya uwanja wakati huo, na aliendelea hivyo kipindi chake chote cha uchezaji.
"Wakati wake Manchester United, alikuwa difenda bora zaidi Ulaya, kama si dunia yote.
“Kumleta hapa QPR – wakati bado ana uwezo wa kutufaa sana kwa ubora wake, kiwango chake, uzoefu wake na tajriba – ni ‘mapinduzi’ makuu kwa klabu.”

No comments:

Post a Comment